WAAJIRI WATAKIWA KUWEKA MAZINGIRA MAZURI YA KAZI KWA WATUMISHI

Na Mwandishi Wetu,Dar es Salaam

WAAJIRI wametakiwa kuweka mazingira mazuri ya kazi kwa wafanyakazi  ili wafanyakazi waweze kufanya kazi  na waone fahari kuitumikia kampuni ama taasisi husika

Akizungumza jijini Dar es Salaam jana katika kikao kazi cha Chama Cha wafanyakazi wa Serikali ,a Mitaa (TALGWU) na waajiri,Afisa Tawala mkuu wa jiji la Dar es Salaam Flora Mgonja alisema waajiri waliopo katika mamlaka mbalimbali wanatakiwa kuwakumbusha maafisa utumishi na wakurugenzi  kuhusu kuwafuatilia na kuwafahamu wafanyakazi wao ili wajue jinsi ya kuwasiliana nao na kutatua matatizo yao.

“Maafisa utumishi na wakurugenzi jambo kubwa sana la umuhimu ni kuwafahamu watumishi wetu unaweza ukamuona mtu kila siku anachelewa kazini kumbe ana matatizo ambayo anapaswa kusikilizwa.

“Tunatakiwa kujua ni namna gani tunaweza kuweka mazingira bora ya watu,wapo watumishi ambao wanaamka asubuhi  hawatamani kwenda kazini kwa sababu ya maafisa rasilimali watu,wakurugenzi ipo sehemu  anaitwa Mungu mtu hii inamfanya mtu achukie kazi,”alisema Mgonja.

Alisema ni muhimu kwa kila ofisi kuweka mazingira mazuri ya kazi  ili mtumishi akiamka atamani kufanya kazi  na kuja kazi.

“Sehemu ya kazi ni sehemu ambayo mtumishi anatakiwa aifurahie ,wito kwa wafanyakazi kuhakikisha anatimiza wajibu wao,”alisema 

Alisema yapo malalamiko pia ya wafanyakazi wanasema mnakaa sana ofisini kuliko kwenda kwenda kwenye vituo vya kazi.

Awali Naibu Katibu Mkuu TALGWU Wandiba Ngocho alisema chama chao ndiyo chama ambacho kinatetea wafanyakazi waliopo chini ya mamlaka ya serikali za mitaa ukiacha walimu kuna kundi kubwa la tunaowatetea.

“Kitu muhimu kinafanywa na chama ni kuwafanya wafanyakazi kuwa karibu sana na wanachama wake,ni utaratibu wetu kama chama tunakutana na wadau hawa kila mwaka mwisho wa siku hii ni kama kioo tunajitathimini kila mwaka.

“Tumefanya hii kila mikoa lakini leo ni zamu ya mkoa wa Dar  es Salaam,tunawashukuru waajiri pamoja na changamoto nyingi lakini tuna uhusiano mzuri,”alisema Ngocho.

Alisema chama huwa kina utaratibu wa mazungumzo wanakaa wanaongea  na waajiri pia kuna watendaji wa mitaa vijiji unataka wafanye kazi kwakutumia kanuni na utaratibu.