KAILIMA:HATUTAONGEZA SIKU ZA KUJIANDIKISHA DAFTARI LA WAPIGA KURA

Na Mwandishi Wetu, Dodoma.

MKURUGENZI wa Uchaguzi, Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Ramadhani Kailima, amewataka Watanzania kuitumia siku ya leo Mei 22, 2025 ambayo ni ya mwisho kujiandikisha katika vituo mbalimbali vya wapiga kura ili waweze kupata haki zao za kupiga kura katika uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika mwezi Oktoba mwaka huu 2025.

Kailima ameyasema hayo wakati alipokuwa anatembelea vituo vya kujiandikisha wapiga kura katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma, katika Jimbo la Dodoma Mjini na Mtumba Mkoani Dodoma, jana Mei 21, 2025.

Kailima pia amekagua zoezi la uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura awamu ya pili, akiangalia zoezi linavyoendelea kufanyika vituoni pamoja na kujua kama kuna changamoto mbalimbali katika vituo hivyo.

‘’Tume ni kuhakikisha kuwa kila Mtanzania mwenye sifa anapata fursa ya kuandikishwa kwa usahihi bila kukosea, licha ya kuwa kuna kituo kuna mtu amekosea majina yake wakati anajiandikisha, hii ni kosa, lazima tuwe makini wakati unahakiki au kujiandikisha vituoni,’’ alisema Kailima.

Kwa upande wake Afisa Mwandikishaji wa Jimbo la Dodoma Mjini na Mtumba, Dickson Kimaro amesema zoezi lilikua la siku saba, kuanzia Mei 16 hadi 22, idadi ya wananchi wanaofika vituoni ni kubwa hivyo amewataka wananchi waendelee kujitokeza siku ya kesho ambapo zoezi litahitimishwa.

Naye Mwananchi aliyefika kujiandikisha katika Kituo cha Kilimani Ofisi ya Mtendaji, amesema amefanikisha kujiandikisha ikiwa ni haki yake ya msingi, na amesema Tume imejipanga vema kufanikisha wananchi wanajiankisha kwa utulivu bila usumbufu naye amefanikisha hilo.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *