Na Asha Mwakyonde,DODOMA
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM), linatarajia kuzindua Ilani ya uchaguzi ya mwaka 2025 kuelekea 2030 ya chama hicho katika
Mkutano Mkuu Maalum na wa kihistoriaTaifa ambao utafanyika Mei 29 na 30, mwaka huu jijini Dodoma.

Hayo yamesemwa leo jijini hapa na Katibu wa Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Amos Makalla wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu tukio kubwa la kihistoria la Mkutano huo amesema Ilani hiyo watakayoizindua ni ya watanzania.
Amefafanua kuwa mkutano una ajenda kuu tatu ambazo ni kupokea taarifa ya utekelezaji Ilani CCM katika kipindi cha miaka mitano kwa serikali Tanzania Bara na Zanzibar.

Katibu huyo amesema ajenda nyingine ni uzinduzi wa Ilani ya uchaguzi wa Chama Cha Mapinduzi kuelekea uchaguzi mkuu 2025 kuelekea 2030 itakayokuwa na mambo muhimu ambayo CCM inakwenda kuyanadu kwa wananchi .
Makala amesema ajenda ya Tatu ni kufanya marekebisho madogo kwenye katiba ya Chama Cha Mapinduzi ambayo yatafahamika siku ya mkutano Mkuu.

“Tumepokea maoni ya wananchi,asasi za kiraia,tumefanya utafiti tunaelewa kiu ya watanzania ilani tunayoenda kuizindua inaenda kukonga nyoyo za watanzania na kwa lugha rahisi yajayo yanafurahisha.” amesema Makalla.
Amos ameeleza kuwa mkutano huo utatanguliwa na vikao vya awali vya kamati kuu ya Chama hicho Mei 26 mwaka huu mada na kufuatiwa na kikao cha Halmashauri Kuu ya Taifa kitakachofanyika mei 28 mwaka huu.
