OFISI YA MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI WARIDHISHWA NA KASI YA UTEKELEZAJI BWAWA LA KIDUNDA

Na Mwandishi Wetu,Dar es Salaam

OFISI i ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, wametembelea mradi wa ujenzi wa bwawa la Kidunda, mkoani Morogoro huku ikisema wana nafasi ya kushauri na kusaidia mambo mbalimbali yakiwemo ya kimkataba.

Mradi wa Kidunda unagharimu kiasi cha Shilingi Bilioni 335, unatarajia kukamilika ifikapo Juni 2026 na kuchangia kuimarisha huduma ya maji mikoa ya Dar es Salaam na Pwani, kuzalisha umeme megawati 20 ambazo zitaunganishwa katika gridi ya Taifa.

Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Bw. Kisamo Fredrick ameongoza ujumbe wa ofisi hiyo kutembelea mradi huo akisema, wao wana nafasi kubwa katika miradi ya kimkakati na kimaendeleo kushauri na kusaidia mambo mbalimbali yakiwemo ya kimkataba ili kuhakikisha miradi inakwenda bila kukwama.

“Niwashukuru DAWASA, wamekua wakitushirikisha mara kwa mara, nafasi yetu ni kupitia maswala mbalimbali katika miradi na kuzuia changamoto zinazoweza kukwamisha miradi kutokea na kusaidia kusukuma miradi iweze kukamilika kwa wakati,” amesema Kisamo.

Kisamo amesena changamoto zilizobainishwa katika utekelezaji wa mradi huu wamezipokea na kwa nafasi yao watashirikiana na wizara zinazohusika kuhakikisha mradi huu haukwami ili uweze kuleta tija.

Kwa upande wake, Msimamizi wa Mradi kutoka DAWASA, Mhandisi Christian Christopher ameshukuru ujumbe huo kutoka ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kutembelea na kusikiliza changamoto zinazokabili.

“Ukaribu wao kwetu ni muhimu sana kwani wanatusaidia kubaini viashiria mbalimbali vinavyoweza kuleta shida na kufanya mradi usitekelezeke kwa wakati.

Haya yote waliotushauri tunayapokea kwa uzito mkubwa na kuanza kuyafanyia kazi mara moja,” amesema Mhandisi Christopher.