Na Mwandishi Wetu,Tanga
Waziri Mkuu, Mhe. Kassim Majaliwa ameipongeza Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kwa kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia hapa nchini.
Mhe. Majaliwa amebainisha hayo leo terehe 16 Oktoba 2025 alipotembelea banda la REA wakati wa Kilele cha Maadhimisho ya Wiki ya Chakula Duniani 2025 yaliyofanyika katika viwanja vya shule ya Usagara jijini Tanga.

Katika hatua nyingine, Mhe. Majaliwa ameipatia tuzo ya pongezi REA ambapo imeibuka kuwa mshindi wa pili wa banda bora katika kuhudumia wananchi katika maadhimisho ya Wiki ya Chakula yaliyofanyika mkoani humo.
Naye, Mhandisi kutoka REA, Ramadhan Mganga amesema Rais Samia ni kinara wa kuhamasisha matumizi ya nishati safi nchini na kuwataka wananchi kuunga mkono jitihada za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan za kuhama kutoka kwenye matumizi ya nishati zisizo safi na salama na kuanza kutumia nishati safi ya kupikia.

Kwa upande wake, Mwakilishi wa REA mkoani Tanga, Mha. Raphael Njango ameeleza kuwa, utekelezaji wa miradi ya REA katika mkoa huo inaendelea ambapo vitongoji 2,382 vimefikiwa na huduma ya umeme sawa na asilimia 52.6 ya vitongoji vyote 4,531.
Wakala wa Nishati Vijijini (REA) umeshiriki katika maadhimisho hayo ambapo imeuza majiko ya gesi kwa bei ya ruzuku ya shilingi 17,500 tu ambapo jumla ya majiko 500 yameuzwa mkoani humo kupitia maonesho hayo.

