HALI YA HUDUMA YA MAJI DAR, PWANI NI SHWARI’

Na Mwandishi Wetu,Dar es Salaam

Wakazi mbalimbali wa Jiji la Dar es Salaam na Mkoa wa Pwani wameridhishwa na hali ya huduma ya maji katika maeneo yao inayozidi kuimarika na hawana hofu juu ya usalama wa huduma hii.

Upatikanaji huo wa maji unaoridhisha ni mkakati wa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA), kuhakikisha kila mtumiaji wa huduma ya maji inanufaisha wananchi wengi eneo lake la kihuduma mikoa ya Dar es Salaam na Pwani.

Wananchi mbalimbali wamezungumzia hali ya upatikanaji wa huduma ya maji ambapo wamepongeza jitihada zinazofanywa na Mamlaka kuhakikisha maji yanapatikana pasipo changamoto yoyote ikiwemo ya usalama.

Ndugu Ibrahim Isanja, Mkazi wa mtaa wa Kilungule, kata ya Kimara amesema huduma ya maji kutoka DAWASA ni muhimu kwao kwani kwasasa hawana mbadala wa huduma hiyo katika eneo lao na ni maji haya wanayotumia siku zote majumbani na kwenye shughuli za kila siku.

“Siku chache zilizopita paiibuka taharuki juu ya usalama wa maji haya tunayotumia hali iliyozua hofu baina ya wananchi, lakini ni maji haya haya tumeendelea kuyatumia kwa kipimdi chote bila kupata madhara yeyote na niipongeze DAWASA kwa kuwa wepesi kutaarifu wananchi maji tunayotumia ni safi na salama kwa matumizi yetu,” amesema Ndugu Ibrahim.

Kwa upande wake, Ndugu Zainabu Issa, Mkazi wa Mbezi amewaondoa hofu watumiaji wa huduma ya maji kutoka DAWASA kuwa maji hayo ni salama kwa matumizi na ndiyo maana hakuna mwananchi yoyote amepata madhara kwa kuyatumia.

“Napenda kuwashauri wananchi wenzangu inapotokea taharuki yeyote tuweze kuwa na subira na kupata taarifa sahihi kutoka kwa wahusika, maji haya ya DAWASA ni safi na salama na tunayatumia kila siku,” amesema Ndugu Zainabu na kuongeza:

Kwa upande wake, Mkazi wa Zinga, Wilaya ya Bagamoyo, Mkoa wa Pwani, Andrew Frank amesema wao hawana changamoto yoyote ya maji kwani yanatoka wakati wote: “Na kubwa si mimi wala majirani zangu ambao wamepata madhara kwa kutumia maji haya.”