Na Mwandishi Wetu,Dodoma
MKURUGENZI wa Nishati Jadidifu na Teknolojia Mbadala wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mha. Advera Mwijage, amesema REA imeanza utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa vituo vidogo vya mafuta vijijini ili kuboresha upatikanaji wa huduma za mafuta na kuchochea maendeleo ya shughuli za kiuchumi katika maeneo ya vijijini.
Akizungumza na wadau waliotembelea Banda la REA katika Maonesho ya Nane Nane yanayoendelea jijini Dodoma, Mha. Mwijage amesema Wakala pia unaendelea kutekeleza miradi ya nishati safi ya kupikia, pamoja na miradi ya nishati jadidifu na teknolojia mbadala, inayolenga kuongeza upatikanaji wa nishati salama, nafuu na endelevu kwa wananchi.

Ameeleza kuwa utekelezaji wa miradi hiyo unalenga kuboresha maisha ya wananchi, kuongeza fursa za biashara na uwekezaji, kulinda mazingira, pamoja na kuchochea ukuaji wa uchumi wa vijijini kupitia matumizi ya nishati bora.
Aidha, amewakaribisha wananchi na wadau kutembelea Banda la REA ili kujifunza zaidi kuhusu utekelezaji wa miradi mbalimbali ya nishati vijijini na fursa zinazotokana na sekta hiyo.



