Na Mwandishi Wetu,Dodoma
MWENYEKITI wa Bodi ya Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST), Bi. Yokbeth Festo Myumbilwa, amesema tafiti za jiosayansi zinazofanywa na taasisi hiyo zina mchango mkubwa katika kuibua maeneo yenye rasilimali za madini, kuvutia uwekezaji na kuchochea ukuaji wa uchumi wa Taifa unaolengwa katika Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
Akizungumza katika Maonesho ya Nanenane, Bi. Myumbilwa amesema jukumu kuu la GST ni kufanya tafiti za jiosayansi zinazobaini maeneo yenye madini na kutoa taarifa sahihi zitakazowezesha wawekezaji kufanya maamuzi ya kuwekeza katika sekta ya madini, hatua ambayo huongeza uzalishaji, ajira na mapato ya Serikali.

Amesema pamoja na sekta ya madini, tafiti za GST zina mchango katika sekta ya kilimo kupitia utambuzi wa madini yanayotumika kurejesha rutuba ya udongo katika maeneo yenye upungufu wa virutubisho. Ameeleza kuwa taasisi hiyo pia hufanya tafiti za kubaini maeneo yenye changamoto ya rutuba ili kuwezesha matumizi sahihi ya rasilimali hizo katika kuboresha uzalishaji wa kilimo.
Bi. Myumbilwa ameongeza kuwa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inalenga kuifikisha Tanzania katika uchumi wa kati wa juu wenye thamani ya takribani dola za Marekani trilioni moja, huku sekta ya madini ikiwa miongoni mwa sekta muhimu zitakazochangia kufikiwa kwa lengo hilo.

Amefafanua kuwa ili kufanikisha azma hiyo, GST imejikita katika kufanya tafiti za kina za jiosayansi ambazo hutoa taarifa muhimu kuhusu maeneo yenye fursa za madini, hivyo kuongeza uwekezaji na kukuza mchango wa sekta ya madini katika Pato la Taifa.
Aidha, amesisitiza kuwa Serikali imeendelea kuonesha dhamira ya kuimarisha shughuli za utafiti kwa kuanzisha mfuko maalumu wa utafiti wa madini utakaowezesha kufanyika kwa tafiti za kina katika maeneo mbalimbali nchini.

Amesema tafiti hizo zitapanua uelewa wa jiolojia ya Tanzania na kusaidia Serikali kubaini maeneo mapya yenye madini, jambo litakalohakikisha uchimbaji unaendelea hata baada ya migodi iliyopo sasa kufikia mwisho wa maisha yake.
Kwa mujibu wake, matokeo ya tafiti hizo pia yataiwezesha Serikali kutenga maeneo mahsusi kwa ajili ya wachimbaji wadogo, wa kati na wakubwa kulingana na taarifa za kisayansi zitakazopatikana, hatua itakayosaidia usimamizi bora na matumizi endelevu ya rasilimali za madini.

Bi. Myumbilwa amewasihi wananchi, wachimbaji na wadau wote wa sekta ya madini kutembelea banda la GST katika Maonesho ya Nanenane ili kujifunza kuhusu huduma mbalimbali zinazotolewa na taasisi hiyo, ikiwemo tafiti za jiosayansi, huduma za maabara, ramani za jiolojia na ushauri wa kitaalamu kuhusu sekta ya madini.


