Na Aziza Masoud,Dar es Salaam
BODI ya Bima ya Amana (DIB), imesema mpaka sasa jumla Sh Bilioni tisa kati ya Bilioni 11 zimeshalipwa kwa wateja waliokuwa wamehifadhi fedha katika benki saba zilizotangazwa mufilisi na Benki Kuu ya Tanzania (BoT) kuwasisitiza wateja kufika katika benki walizotangaziwa kuchukua fedha zao.
Akizungumza katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa Dar es Salaam,Afisa Mwandamizi DIB Silvan Makore alisema fedha hizo zinalipwa kupitia benki ambazo zimepewa kandarasi za kusimamia malipo hayo DIB kutokana na bodi hiyo kutokuwa na matawi katika maeneo mengi.

“Kuna benki tuliziteua kwa ajili ya wateja wanaoidai bima ya amana,wateja ambao walihifadhi fedha zao katika benki zilizofilisiwa kamaa benki ya biashara TCB inalipa wateja wanaodai bima ya amana,tuliona DIB ni busara ili mwananchi asipande gari akitumia fedha nyingi kupata fedha zake kwajuja kwenye matawi yetu yaliyopo Dar es Salaam na Dodoma.
“Mteja akifika benki husika atatoa kitambulisho atatambuliwa na wafanyakazi wa TIB atajazishwa fomu na kulipwa fedha zake pia wateja waliokopa kwenye benki zilizofungwa wanalipa malipo yao kupitia NMB kwakuwa benki ipo nchi nzima ,”alisema Makore.

Alisema kati ya benki saba zilizofungwa 2018 kiwango cha fidia kilikuwa Sh bilioni 11 na mpaka sasa wameshalipa Sh Bilioni tisa sasa zimebaki bilioni tatu hazijachukuliwa na wateja.
Alisema fedha hizo zilizobaki ni nyingi hivyo wateja waliokuwa kwenye benki hizo ni vyema wakaenda kuzichukua kwakuwa ikifika miaka 15 hazijachukuliwa zinarudishwa serikalini
Akizungumzia kuhusu usalama wa fedha kwa wateja katika baadhi ya benki Makore aliwatoa wasiwasi wananchi ambao wanahofia kuhusu fesha zao na kusisitiza kuwa kila benki inalipa kiasi cha fedha DIB kwa ajili ya ulinzi wa fedha za wateja.

“Ukiwa mteja wa benki wewe ni mteja wa bima ya amana ukiweka pesa benki ujue huko unalipiwa hata ikitokea Benki Kuu ikafungia benki yako unapaswa kujua kuwa upo salama.
“Na sisi kila baada ya miezi tunahakikisha wanakuja kuleta ripoti yao ya ukaguzi uendeshaji wa robo mwaka au mwaka mzima tuone kama benki yako inapata faida au hasara,hata mteja una wajibu wakufuatilia ripoti hizo na ukiona mwenendo sio mzuri unafumgua akaunti benki nyingine,”alisema Makore.
Alisema mteja pia una uwezo wakuhoji kwa nini benki husika wamepata hasara na wahusika watatoa sababu na watakwambia jitihada wanazofanya kuongeza faida.
Amewataka wananchi ambao hawana uelewa wa masuala ya amana za benki kufika katika banda hilo kupatiwa elimu hiyo.


