TEMEKE YAONGOZA WARAIBU HEROIN DAR ES SALAAM

Na Mwandishi Wetu,Dar es Salaam

MAMLAKA ya Kupambana na Kudhibiti Dawa za Kulevya (DCEA) imesema wilaya ya Temeke ina watu 2500  wanaotumia dawa tiba za methadone kutokana na matumizi ya heroin jambo linalosababisha wilaya hiyo kuongoza kwakuwa na  waraibu wengi mkoan Dar es Salaam.

Akizungumza katika tamasha la kupinga dawa za kulevya lililofanyika  viwanja vya Mwembe Yanga Temeke kwa niaba ya  Kamishna Jenerali wa DCEA Aretas Lyimo ,Kamishna Divisheni ya Kinga,Tiba na Huduma na Utengemao  Dk.Cassian Nyandindi amesema wilaya ya Temeke inaongoza kwakuwa na watu waliopata tatizo ya  uraibu kwa mkoa wa Dar es Salaam  huku wilaya za Kinondoni,Ilala,Ubungo na Kigamboni zikifuata.

“Tatizo la dawa za kulevya ni kubwa kwa Dar es Salaam kwa wilaya zote lakini wilaya ya Temeke inaongoza kwakuwa katika eneo hili tatizo ni kubwa kwakuwa watu 2500 waliokuwa wakitumia dawa za kulevya aina ya heroin wanatumia huduma ya methadone,idadi hiyo ni idadi kubwa kiwilaya,”alisema Dk.Nyandindi.

Alisema mbali na kutumia methadone  pia waraibu 16000 wamepatiwa huduma ya tiba ya tibiwaafya ya akili kwa wilaya ya Temeke kwa mwaka 2014.

Alisema kutokana na hali hiyo  matamasha hayo ni muhimu kwakuwa yanasisitiza uwepo wa tatizo la  dawa za kulevya na kwamba si jambo la mtu mmoja bali ni la jamii nzima.

“Ninachopenda kusisitiza ni kwamba tatizo la dawa za kulevya haliwezi kumuacha mtu salama,kama halitakugusa mtu binafsi litamgusa mwanafamilia majirani na jamii kwa ujumla,sisi sote tunatakiwa kupiga vita dawa za kulevya,kila mwaka DCEA uhamasisha kushiriki kupambana na dawa za kulevya,”alisema Dk.Nyandindi.

Alisema  matamasha hayo  pia  hufanyika kikanda ambapo kuna  kanda ya Mashariki,kanda ya ziwa na Nyanda za Juu Kusini na Mtwara pamoja na  Kanda ya Kusini.

Naye Mkuu wa wilaya ya Temeke Sixtus Mapunda ambaye  alikuwa mgeni rasmi wa ghafla hiyo alisema wilaya hiyo imekuwa na idadi kubwa ya waraibu wa madawa ya kulevya kutokana na haiba ya watu wa eneo hilo.

“Temeke ni rahisi sana kutumika katika matumizi na usambazaji,jiografia yetu na mazingira ni rafiki sana kwenye kusambaza na kutumia,kutuletea ghafla hii Temeke ni fursa ya watu kupata elimu.

“Kuna watu wapo wamezunguka wanasikiliza hapa inaonyesha namna gani suala hili la madawa ya kulevya ni seriuos nchini,bahati mbaya maangamizi yake ni ya muda mrefu  watumiaji wanakutana tu matokeo  ambayo kupona kwake sio rahisi,”alisema Mapunda.

Alisema ni muhimu  kupambana na madawa ya kulevya katika ngazi zote lakini pia jamii ikitaka kumaliza kabisa dawa zakulevya kwa njia rahisi kukata mnyororo wa usamabazaji ambayo ni ngumu kwakuwa unawaza unaanzia wapi kwenye kiwanda kusafirisha au yanapohifadhiwa.

“Kuna ugumu wakukata supply kwa sababu haina njia moja wala formula moja,la pili kupambana na yule anayeenda kutumia kwakuwa  tusipokuwa na watumiaji mzigo hautafika,tukikata watumiaji mzigo hautafika mtaani kwa sababu utakuwa hauna soko,”alisema Mapunda.

Alisema kutokana na mapambano la tatizo hilo kuwa kubwa ni wakati wa wazazi kuongea na watoto wao mapema kuhusu dawa za kulevya na madhara yake ili kupunguza wimbi la  watumiaji.

“Watoto wanapaswa kuambiwa sio kila jambo ni la kujaribu,vitu havijaribiki wala wasionje kwa sababu vitawapeleka sehemu ambayo  hawatoweza kutoka wala  kurudi nyuma,”alisema Mapunda.

Naye mmoja wa waraibu ambaye amepata nafuu na kuanzisha kituo Sura Nyembo alisema alianza kutumia dawa za kulevya aina ya heroin mwaka 2000 na kuacha mwaka 2013 kupitia nyumba za kujitibu.

“Nimetumia heroin kwa miaka  13  kupitia nyumba hizi za kujitibu nilibahatika  kuondokana na matumizi haya,jamii inatakiwa kujua madawa ya kulevya sio kitu kizuri,mimi niliacha  hadi masomo,”alisema Nyembo.

Alisema  ili kuondoa tatizo la matumizi ya dawa za kulevya kuna haja kuhakikisha watumiaji wanapungua ili kupunguza uhitaji  utakaoondoa usamabazaji.

Alisema pamoja na utumiaji wa dawa za kulevya kuenea pia kwa sasa kumekuwa na wimbi la watu wanaotumia bangi aina ya skanka.