Na Mwandishi Wetu,Mbeya
Mganga Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Dkt. Elizabeth Myema, ameipongeza Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali k⁹wa kutoa huduma bora kwa jamii huku akiitaka Mamlaka kuendelea kuwajengea uwezo wadau wanaojihusisha na Tiba Asili kwa kuzalisha dawa zenye ubora kwa kuwa sehemu kubwa ya watanzania wanatumia dawa hizo.
Dkt. Myema ameyasema hayo leo wakati alipotembelea banda la Mamlaka katika Maadhimisho ya wiki ya Tiba Asili ya Mwafrika yanayofanyika katika viwanja vya Uhindini mkoani Mbeya.

“Niwapongeze Mamlaka ya Maabara ya Mkemia mkuu wa Serikali kwa kutoa huduma bora na nzuri kwa watanzania,lakini niseme tu kwamba muendelee kuwajengea uwezo wadau hawa wa Tiba Asili, muwasaidie ili Dawa zao ziweze kupita kwenu ziweze kuchunguzwa na kutumika kwa sababu sehemu kubwa ya watanzania wanatumia Tiba Asili kwa hiyo Dawa zitakapochunguzwa na kupimwa watumiaji watakua salama.” alisema Dkt. Myema.
Akizungumzia hatua hiyo Kaimu Meneja wa Maabara ya Chakula na Dawa, Everlight Matinga, amesema Mamlaka inatekeleza na inaendelea kutekeleza jukumu hilo la kuwajengea uwezo wadau wa Tiba Asili kuwapa elimu pamoja na kuwashauri kuzifanyia uchunguzi Dawa ili kuhakiki ubora na usalama wake.

“Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali imekua ikitekeleza jukumu hilo la kuwapa uelewa wadau hawa kuhusiana na mbinu bora na salama za uchakataji wa Dawa Asili hizo, na ni muendelezo ambao upo na tumekuwa tukifanya hivyo katika maadhimisho mbalimbali ya Tiba Asili katika kila mkoa na ndio maana hata mwaka huu tuko hapa kuhakikisha wadau hawa wanapata elimu sahihi kuhusiana na uchunguzi wa kimaabara wa Dawa hizo” alisema Matinga.
Kwa Upande wake mdau wa Tiba Asili ambae ni Mkurugenzi kutoka kampuni ya Iphytos, Dkt. Shadrack Maduru, amesema ni muhimu sana Dawa za Asili kufanyiwa uchunguzi wa Kimaabara ili kutambua ubora wake lakini pia kuzingatia usalama wa kila mtumiaji ili kuendelea kuboresha Afya zao.




